WADAU WATAKIWA KUSHIRIKI KUMALIZA MGOGORO DRC
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa katika picha pamoja na pamoja wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika katika ukumbi wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2025.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Mkutano wa pamoja wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika katika ukumbi wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2025. Mkutano huo pamoja na mambo mengine unajadili hali ya ulinzi na usalama Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Na Mwandishi Wetu - Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Rais wa Kenya, Dk William Ruto amesema mazungumzo ya kidiplomasia yatamaliza vita vinavyoendelea katika mji wa Goma nchini DR Congo.
Vita vinavyoendelea mjini Goma nchini DR Congo vimesababishwa na Kundi la Waasi la M23 ambapo hadi sasa inadaiwa zaidi ya watu 3,000 wamepoteza maisha.
Rais Ruto amesema hayo leo Ikulu jijini Dar es Salaam, wakati akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano wa Pamoja wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa EAC na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC)
Rais Ruto amesema DRC imepitia wakati mgumu kwa muda mrefu na kuweka bayana kuwa inatosha kwa sasa, hivyo kuwataka viongozi wenzake kushikamana kuhakikisha hali hiyo inakoma.
"Historia inaonesha DRC imepitia kwenye misukosuko kwa muda mrefu, nadhani tanapaswa kuchukua hatua sasa, kwani mgogoro huo unaweza kutatuliwa, unapaswa kutatuliwa na ni lazima utatuliwe kwa njia ya mazungumzo ya kidiplomasia," amesema.
Mwenyekiti huyo wa EAC amesema kwa hali ilivyo sasa amani ya DRC haiwezi kupatikana kwa njia ya nguvu, bali mazungumzo.
Amesema ni lazima pande zote zinazopingana kukutanishwa na kuzungumza ili kuhakikisha DRC inakuwa na amani na umoja.
Amesema kutokana na vita vinavyoendelea DRC wananchi wake wamekuwa wakiuwawa, kukosa haki za kufanya shughuli za uzalishaji, kwani muda wote wapo kama wakimbizi.
Mwenyekiti huyo amesema katika historia ya kuanzishwa EAC na SADC leo ndio mara ya kwanza viongozi wakuu wa serikali hizo kukaa pamoja kuzungumza kuhusu utatuzi wa mgogoro, hivyo imani yake ni kuona kikao hicho kinakuwa na matokeo chanya kuhusu DRC.
"Naomba tutumie mkutano kuleta suluhu ya Goma na DRC kwa ujumla, leo tumeweza kukaa pamoja sisi EAC na SADC imani yangu ni kupitia kikao hiki tunaenda kuandika historia ya kipekee," amesema.
Rais Ruto amesema vita vinavyoendelea DRC vina madhara duniani kote, hivyo ni lazima mbinu zote sahihi kutumika kuleta amani.
Aidha, Rais Ruto alitumia nafasi hiyo kuwataka wadau wote wakiwemo asasi za kiraia, mashirika ya kimataifa na wengine kuungana na serikali za EAC na SADC kumaliza mgogoro huo ambao umesababisha wananchi wasio na hatia kuteseka na kuwauwa.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa SADC na Rais wa Zimbabwe, Dk Emerson Mnangagwa amesema kinachoendelea DR Congo kinapaswa kuwaunganisha Waafrika kama ilivyokuwa wakati wakutafuta uhuru kwa nchi zao.
Rais Mnangagwa amesema Waafrika wanapaswa kuungana na kuhakikisha watu wao wakiwemo wananchi wa DRC wanakuwa salama.
"Naungana na Rais Ruto katika kuwaomba viongozi na wadau wote kuhakikisha tunaunga kumaliza mgogoro wa DRC na kwingineko," amesema.
Mwenyeji wa mkutano huo na Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC (SADC - Organ Troika), Rais Samia Suluhu Hassan amesema amefarijika kuona mwitikio mkubwa wa viongozi kushiriki mkutano huo na kwamba kinachoendelea DR Congo hakikubaliki na ni wakati wa kufikia mwisho.
"Tusipochukua hatua kwa sasa historia itatuhukumu, kwani wananchi wa DRC wanateseka, wanashindwa kufanya shughuli za kijamii na kiuchumi, hivyo kupitia mkutano huu tunapaswa kufungua ukurasa mpya kwa wananchi hao," amesema.
Amesema Tanzania ipo tayari kutoa ushirikiano wa kila aina kuhakikisha DRC inakuwa salama, kwani nchi hiyo ni muhimu katika ukanda wa EAC na SADC.
Rais Samia amssema imani yake ni kuona kikao hicho kinaenda kutoka na maazimio ambayo yatawezesha wananchi wa DRC wanaanza maisha mapya ya umoja na amani.
Mkutano huo wa leo umehudhuriwa na Rais Samia Suluhu Hassan, Emerson Mnangagwa, William Ruto, Hassan Sheikh Mohamud, Paul Mahame, Yoweri Museveni, Hakainde Hichilema, Moussa Faki wa Umoja wa Afrika (AU), Waziri Mkuu wa Burundi Gervas Ndirakobuca, mawaziri kutoka Angola, Sudan, Sudan Kusini, Malawi, Afrika Kusini na Madagascar.
No comments