CCM YAELEZA SIRI YA USHINDI, YATOA NENO KWA WAPINZANI 2020
Ikiwa
zimepita siku mbili baada ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kuibuka na ushindi wa
Kata 19 kati ya 20 na Jimbo la Dimani, katika uchaguzi wa marudio uliofanyika
Januari 22, 2017.
Kimeeleza
siri za ushindi huo, huku utendaji kazi wa Serikali ya Awamu ya tano chini Rais
John Magufuli ukitajwa kuwa kivutio cha wananchi wengi kupigia kura wagombea wa
CCM.
Akizungumza
na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Katibu wa Itikadi na Uenezi
CCM, Humphrey Polepole amesema siri nyingine ya ushindi huo ni utekelezwaji wa
ahadi zilizomo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ikiwa ni pamoja na ahadi ya
ujenzi wa uchumi wa viwanda, elimu bure kuanzia darasa la kwanza hadi kidato
cha nne, vita dhidi ya ufisadi, rushwa na ubadhirifu wa mali za umma pamoja na
ununuzi wa ndege mbili za shirika la ndege ambazo zinachangia ukuaji uchumi wa
nchi na sekta ya utalii.
"Vita
dhidi ya ufisadi na rushwa inayotekelezwa na serikali ya awamu ya tano,
utekelezwaji wa ahadi zilizoahidiwa katika kipindi cha kampeni za uchaguzi
2015, ndio siri kuu mbili za ushindi wa CCM," amesema.
Pia
Polepole amejibu tuhuma za Chama cha Wananchi (CUF)dhidi ya CCM ambapo
iliituhumu CCM kuwa imeshiriki kuvuruga uchaguzi na kuiba kura na kwamba ndio chanzo cha Mgombea wake katika
jimbo la Dimani, Abdulrazak Ramadhani kushindwa.
Polepole
amekana tuhuma hizo na kuitaka CUF kujitafakari ilipoanguka badala ya kulaumu
chama chake.
Matokeo
ya Dimani yamedhihirisha CUF ilikua tatizo tangu uchaguzi uliopita, 2015 CCM
ilipata kura 4400, CUF 2300, 2017 CCM
imepata kura 4860 sawa na asilimia 78, CUF wamepata 1200 anguko la zaidi ya
50%. CUF wamtafute mchawi juu ya kushindwa na anguko lake yuko ndani ya chama
chao hasa Zanzibar," amesema.
Aidha,
Polepole ametuma salamu kwa vyama vya upinzani juu ya uchaguzi mkuu ujao wa
mwaka 2020, ambapo amesema chama chake kiko katika hatua ya kujiimarisha pamoja
na kufanya uchaguzi wa viongozi.
"Baadhi
ya wanasiasa wanatutisha kwamba 2020 tutakutana na tutaachia madaraka, kama
wanatutabiria giza, kwetu CCM tuna mwanga mkubwa unaotupa hamasa ya kuwatumikia
watanzania kwa moyo, uadilifu, umoja ili kuwaletea maendeleo ya haraka,"
amesema
No comments