Breaking News

WANANCHI WAHAMASHWA KUSHIRIKI MATEMBEZI YA HISANI KUCHANGIA WAHANGA WA TETEMEKO LA KAGERA

Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kasiga

Na. Immaculate Makilika- MAELEZO

Wizara ya Mambo ya Nje  na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na  Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa matembezi ya hisani ili kusaidia wahanga waliokumbwa na maafa ya  tetemeko  la ardhi lilitotokea  Septemba 10 mwaka huu, huko mkoani  Kagera.

Akizungumza  na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kasiga amesema kuwa, matembezi hayo ya hisani ya kilomita tano yataongozwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili Alhaji Ali Hassan Mwinyi.

Aliongeza kuwa Matembezi hayo yatafanyika siku ya Jumamosi Septemba17 mwaka huu, ambapo yataanzia Bwalo la Polisi Osterbay (Polisi Officer’s Mess) kuanzia saa 12 asubuhi.

Aidha amesema kuwa, matembezi hayo yana lengo la kuhamasisha wafanyabiashara, taasisi za fedha, kampuni mbalimbali pamoja na  jamii ya watanzania, wanadiplomasia waliopo nchini kuchangia kwa kutoa misaada mbalimbali ili kusaidia wahanga maafa ya tetemeko la ardhi la mkoani  Kagera.

“Tunafanya kampeni hii ya tembea kwa ajili ya Kagera, kwa lengo la kuwahamasisha watanzania, wafanyabashara na jumuiya ya wanadiplomasia waliopo nchini ili kila mtu aweze kushiriki kwa kuchangia kiasi chochote cha fedha kitakachosaidia wenzetu waliokumbwa na maafa ya tetemeko la ardhi lililotokea Kagera” alisema Kasiga

Hivyo basi, Wizara hiyo imeeandaa daftari maalumu la michango kwa jumuiya ya mabalozi  katika nchi zote zenye Ofisi za Ubalozi wa Tanzania, ili kuunga mkono zoezi la kuwasaidia wahanga wa maafa ya tetemeko la ardhi lilitokea mjini Bukoba.

Pia Serikali imefungua akaunti rasmi kwa jina la Kamati Maafa Kagera katika benki ya CRDB ya mkoani Kagera yenye namba 0152225617300 ambayo itakayotumika kupokea  michango kutoka kwa watu mbalimbali.


No comments