Breaking News

RAIS MWINYI: BANDARI YA MANGAPWANI INALENGA KUTOA HUDUMA KWA UKANDA WOTE WA AFRIKA MASHARIKI

Jakarta, Indonesia
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) iko tayari kushirikiana na Shirika la Pelindo kujenga Bandari Jumuishi ya Mangapwani ambayo itajumuisha sehemu ya kuhifadhi nafaka, makontena, bandari kavu, chelezo pamoja na hifadhi ya mafuta.

Pia, bandari hiyo Jumuishi ya Mangapwani inalenga kuwa kituo cha kuhudumia eneo la ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika ijulikanayo kama Trans-shipment Port.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo leo alipotembelea Bandari ya Tanjung Priok iliopo Jakarta na kukutana na uongozi wa Shirika la Pelindo linalomilikiwa na Serikali ya Indonesia ambalo linaendesha shughuli zote za bandari nchini humo.
Rais Dk. Mwinyi amesema anatambua kuwa Indonesia na Zanzibar zinafanana kwa kuwa ni nchi za visiwa na hutegemea bahari kwa shughuli za usafirishaji.

Aidha, amesema Muundo huo wa kijiografia wa visiwa una changamoto mbalimbali za usafirishaji hivyo bandari inachukua nafasi muhimu katika kutatua changamoto za kibiashara pamoja na kuchochea kupanda kwa uchumi wa nchi.

Naye, Bw. Arif Suhartono Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Pelindo ambalo lina matawi 71 nchini humo likijumuisha kisiwa cha Sumatra kwa upande wa magharibi hadi mashariki ya Papua amesema ziara hii iwe mwanzo wa ushirikiano wa karibu zaidi na kuweka misingi ya ushirikiano wa kimkakati kati ya Indonesia na Zanzibar.

Rais Dk. Mwinyi amekamilisha ziara yake nchini humo iliyoanzia tarehe 01-03 Septemba 2024 katika kisiwa cha Bali ambapo alimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Pili wa Jukwaa la Indonesia na Afrika.





No comments