Breaking News

KAMISHNA DORIYE AKUTANA NA MADIWANI NA VIONGOZI WA MILA NGORONGORO KUIMARISHA UHUSIANO

Na Kassim Nyaki, NCAA.
Kamishna wa Uhifadhi wa mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) Dkt. Elirehema Doriye tarehe 26 Septemba, 2024 amefanya kikao cha kuimarisha uhusiano kati ya mamlaka hiyo, viongozi pamoja na wananchi wanaoishi katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.

Kikao hicho kilichohusisha Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, Madiwani wa kata zote 11 za Tarafa ya Ngorongoro, viongozi wa mila (Malaigwanan) na menejimenti ya NCAA kimelenga kujadili masuala mbalimbali kwa lengo la kuimarisha uhusiano na kutatua changamoto zilizopo ili kuimarisha shughuli za uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii.

“Kikao hiki ni sehemu ya NCAA kukutana na makundi mbalimbali kwa ajili ya kuboresha uhusiano na kuainisha changamoto zilizopo ili tuzitatue na tuendelea kuimarisha shughuli za uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii hasa kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi waliopo sambamba na kuendelea kuwaelimisha kuhama kwa hiari ndani ya hifadhi” alibainisha Dkt. Doriye.
Mbunge wa jimbo la Ngorongoro Mhe. Emmanuel Ole Shangay amempongeza kamishna wa Uhifadhi NCAA Dkt Elirehema Doriye kwa kuendelea kuimarisha uhusiano na wananchi wa Ngorongoro hali inayosaidia kutatua kero za wananchi hao sambamba na kuimarisha uhifadhi shirikishi kwa manufaa ya wananchi hao na watanzania kwa ujumla.  

Mhe. Shangay ameishukuru Serikali kupitia NCAA na Halmashauri ya Wilaya Ngorongoro kwa kuendelea kuimarisha huduma za kijamii kwa wananchi wa Ngorongoro na kutatua changamoto za muda wa wananchi kuingia ndani ya hifadhi kutoka saa 10:30 jioni hadi saa 12 kamili jioni. 

Ameinisha kuwa hakuna kiongozi anayepingana na agizo la serikali kwa wananchi wa Ngorongoro ambao wako tayari kuhama kwa hiari ndani ya hifadhi hiyo kwenda Kijiji cha Msomera na maeneo mengine yaliyotengwa na Serikali na yale wanayochagua wenyewe lakini pia amesisitiza umuhimu wa serikali kuendelea kutoa huduma kwa wananchi ambao bado hawajafanya maamuzi ya kuhama.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro Bw. Sadick Mbilu amefafanua kuwa halmashauri ya Ngorongoro itaendelea kushirikiana na NCAA kuimarisha shughuli za uhifadhi na kutoa huduma za kijamii kama afya, elimu, maji, miundombinu na kukutana na wananchi kwa ajili ya kuwasikiliza, kutatua changamoto zao sambamba na kuendelea kutoa elimu ya kuhama kwa hiari ndani ya hifadhi hiyo kwa ajili kuimarisha shughuli za uhifadhi na kuboresha Maisha ya wananchi nje ya hifadhi.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ngorongoro Mhe. Marekani Bayo ameeleza kuwa halmashauri ya Ngorongoro kupitia baraza la madiwani itaendelea kushirikiana na NCAA katika kukuza uhusiano na kufanya uhifadhi shirikishi kupitia vijiji vyote vinavyozunguka hifadhi ya Ngorongoro na pori la akiba la Pololeti ili wananchi wanufaike na mapato yatokanayo na shughuli za utalii kwa ajili na kuiwezesha Serikali kuwahudumia

No comments