Spika Ndugai Aula. Achaguliwa Kushika Wadhifa Mzito Afrika
Ofisi ya Bunge inapenda kuuarifu umma kuwa Spika wa Bunge Mhe.
Job Yustino Ndugai (Mb), amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Maspika
na Viongozi wa Bunge katika Umoja wa Mabunge ya Jumuiya ya Madola Barani
Afrika.
Uchaguzi huo umefanyika katika Mkutano wa Maspika wa
Mabunge ya Jumuiya ya Madola Barani Afrika uliomalizika jana Mjini Abuja.
Kwa wadhifa huo, Mhe Ndugai ataongoza Maspika wenzake toka
Mabunge na Mabaraza ya kutunga Sheria 63 yaliyoko katika nchi 18 za
Jumuiya ya Madola kwenye Bara la Afrika.
Wadhifa huo ni wa miaka miwili kuanzia sasa hadi mwaka 2019
kutakapofanyika uchaguzi mwingine.
Nchi wanachama wa Umoja wa Mabunge Barani Afrika ni pamoja na
Afrika ya Kusini, Botwana, Cameroon ,Ghana, Kenya, Lesotho,
Msumbiji, Mauritius, Malawi, Nigeria, Namibia, Rwanda, Seychelles, Sierra
Leone, Swaziland, Tanzania, Uganda na Zambia.
Akizungumzia uchaguzi huo, Mhe Ndugai amesema "Kwa hakika nawashukuru Maspika
wenzangu kwa kunipa dhamana hii ya kuwa Mwenyekiti wao, ni heshima kwangu
binafsi lakini zaidi Kwa Tanzania. Ni matumaini yangu kwamba Bunge letu
litaendelea kung'ara kitaifa na kimataifa tukiwa Bunge moja lenye Upendo na mshikamano".
Huu ni wadhifa wa nne kwa Mhe. Ndugai katika masuala ya Bunge
kwenye medani ya Kimataifa. Amewahi kuwa Mwakilishi wa Nchi za Afrika Mashariki
katika Kamati ya Utendaji ya Umoja wa Mabunge ya Jumuiya ya Madola Duniani
mwaka 2008-2011, Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jamii ya Umoja wa Mabunge ya
Afrika, Pacific na Carribbean na Jumuiya ya Ulaya mwaka 2011-2014 na Rais
wa Baraza la Mabunge ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC – PF)
Imetolewa na:
Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano
Ofisi ya Bunge
DODOMA
No comments