Breaking News

Mbunge wa Ubungo mhe Kubenea Akabidhi Madawati 240 kwa shule za Jimbo lake

MBUNGE wa Ubungo Saed Kubenea amekabidhi madawati 240 kwa shule za msingi na sekondari zilizopo katika jimbo hilo lenye kata nane.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi madawati hayo iliyofanyika katika shule ya Sekondari Mashujaa Sinza Parestina jijini Dar es Salaam, alisema shule nyingi zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa madawati.

“katika kukabiliana na changamoto hii Ofisi ya Mbunge imetoa madawati 330, na katika hayo madawati 240 yamekabidhiwa leo kwa hiyo bado madawati 90 yako kwenye mchakato wa kuweza kuyakabidhi, ,” alisema Kubenea.
Alitaja shule zilizopata mgao huo wa madawati kwa upane wa shule za Sekondari kuwa ni Makurumla, Manzese, Makoka, Mgabe ambazo zote zimepatiwa viti na meza 30 huku akiahidi kuipatia shule ya Mashujaa madawati 50 kabla ya mwezi huu wa Februari, 2019 kwisha.

Kwa uapande wa shule za msingi ni Ubungo Plaza, Muungano na Golani ambazo zote pia zimepatiwa viti na meza 30.

Kubenea alisema kuwa madawati hayo yanagharimu sh.milioni 28.8 ambazo zimetoka kwenye mfuko wa jimbo.
Mbunge huyo akiambatana na kamati ya mfuko wa jimbo la Ubungo walitumia siku ya jana pia kufanya ziara yeye akiwa kama mwenyekiti kukagua matatizo yaliyopo kwenye shule za msingi na sekondari.

Pia kamati iliangalia mairadi iliyotekeleza katika mwaka huu wa fedha 2018/2019 na sehemu ya mwaka wa fedha  2017/2019 na miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa shule mbili za sekondari na msingi za Kimara na mradi wa maji.

Awali Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Mashujaa Eda Kondo, akisoma risala alitaja mahitaji ya shule hiyo kuwa ni ujenzi wa uzio, vyumba 17 vya madarasa, Photocopy Machine na Kompyuta.

Kutokana na mahitaji hayo kuwa mengi Kubenea alitoa ushauli wachague vipaumbele vya mahitaji yao ili kuyaandikia barua ya maombi ili maombi hayo yaweze kujadiliwa kwenye kikao cha kamati cha wiki ijayo Jumatatu ya Fubruari 18, 2019.

No comments