Wakili Ajitoa Kesi Ya Uchochezi Ya Mhe Lema.
Wakili Sheck
Mfinanga amejitoa kumwakilisha mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema
katika kesi ya uchochezi akidaiwa kumkashifu Rais John Magufuli akisema
haridhishwi na mwenendo wa shauri hilo.
Mfinanga amejitoa
ikiwa ni siku chache baada ya hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Arusha, Patricia
Kisinda aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo kujitoa kutokana na kuwekewa pingamizi
na upande wa Jamhuri kuwa ana urafiki na Neema ambaye ni mke wa Lema.
Mbele ya Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Arumeru, Desdery Kamugisha, wakili huyo
amesema moja ya sababu ni kutokana na upande wa utetezi kutopewa jalada la
mwenendo wa kesi licha ya kuwasilisha maombi mara tatu mahakamani hapo.
“Kwa kuwa
nimeshaleta notisi ya kukata rufaa naomba iingie kwenye rekodi, najitoa
kuendelea kumwakilisha mteja wangu kutokana na kile ninachokiona kisheria
kwamba tumeomba proceedings (mwenendo wa kesi) na imeshindikana. Mimi si wakili
wake tena, nimejitoa,” amesema.
Baada ya ombi
hilo, Mfinanga alikusanya nyaraka zake, alimuaga mteja wake na kunyanyuka
kwenye kiti alichokuwa ameketi na kutoka ndani ya chumba cha Mahakama.
Hakimu Kamugisha
alimpa nafasi Lema ya kuzungumza naye alisema amemsikiliza wakili wake na hana
pingamizi juu ya ombi hilo.
Hata hivyo,
amesema kwa ufahamu wake ni kwamba, hii ni mara ya tatu upande wa utetezi
umeomba jalada la mwenendo wa kesi lakini hawajapewa na kwa sababu hiyo hana
imani na hakimu.
“Mheshimiwa
nilishasema sina imani na wewe kama mtu niliyekuwa nimemwajiri kunisaidia
katika masuala ya kisheria anaweza kutilia shaka na nilisema hadharani, basi
naomba nipewe muda wa kutafuta wakili mwingine,” amesema.
Lema amesema
anaomba kupatiwa nyaraka zote za kesi na muda wa kutafuta wakili mwingine.
Baada ya ombi
hilo, Wakili wa Serikali, Khalili Nuda alisema ni haki ya kikatiba ya mshtakiwa
kuwakilishwa mahakamani. Aliiomba mahakama impatie muda wa kutafuta wakili
mwingine.
Nuda ameiomba
Mahakama impatie mshtakiwa muda muafaka wa kutafuta wakili mwingine.
Hakimu Kamugisha
amesema wakili wa mshtakiwa amejitoa wakati kesi ilipotajwa kwa ajili ya
kusikilizwa, hivyo Lema anapewa muda wa kutafuta mwingine. Aliahirisha shauri
hilo hadi Novemba 14.
No comments