Breaking News

LHRC KUPINGA KUONGEZWA MUDA WA LESENI YA UZALISHAJI UMEME KWA KAMPUNI YA IPTL

Image may contain: 1 person, sitting
TAMKO KWA VYOMBO VYA HABARI
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu ni shirika lisilo la kiserikali lenye maono makuu ya kuona Jamii yenye Haki na Usawa Tanzania. Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kimejikita katika utetezi wa Haki za Binadamu ikijumuisha haki za maendeleo. 
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kwa mshangao na masikitiko makubwa kinapingana na hatua ya Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA) kupokea na kutangaza kupitia gazeti la serikali la Daily News, la siku ya Jumatano Juni 7, 2017 kusudio la kuiongezea leseni ya uzalishaji umeme kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), kampuni ambayo inahusishwa na kashfa nzito ya uchotwaji wa mabilioni kupitia akaunti ya ESCROW. 
Ikumbukwe kwamba Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) mwaka 2014 ilitoa mapendekezo mbali mbali juu ya umiliki wa mitambo ya IPTL ikiwemo, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufanya uchunguzi juu ya umiliki na uwepo wa rushwa katika utendaji kazi wa IPTL na wabia wake.
Mapendekezo ambayo mpaka sasa hayajafanyiwa kazi huku umma wa watanzania ukiachwa katika bumbuwazi.
Mbali na kutokuwepo kwa taarifa sahihi juu ya upotevu mkubwa wa fedha za watanzania katika sakata la ESCROW, tumeshangazwa na kitendo cha EWURA kutaka maoni ya wadau huku ikiwa inafahamu fika kuwa mikataba kati ya Serikali na IPTL ni ya siri na hivyo wadau hawana sababu za kimkataba za kutoa mapingamizi au maoni. 
Kutokana na sintofahamu hii, Chombo hiki chenye mamlaka ya udhibiti wa Nishati na Madini kilipaswa kujiridhisha juu ya mapendekezo ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Kamati ya Hesabu za Serikali juu ya utata wa umiliki wa IPTL na kashfa za rushwa zinazoizunguka badala ya kutaka maoni au mapingamizi kutoka kwa wananchi na wadau ambao hawajui undani wa mkataba wa IPTL na Serikali.
Kwa kuzingatia misingi ya uwajibikaji wa Serikali na makampuni, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinatoa mapendekezo yafuatayo: 
1. EWURA kusitisha mara moja kusudio hili la kukusanya maoni ya kuiongezea muda kampuni ya IPTL mpaka serikali itakapotekeleza mapendekezo yote ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia kamati yake ya mwaka 2014.
2. EWURA kujiridhisha uhalali wa kisheria juu ya umiliki, kujiridhisha pasipo shaka ushiriki wa IPTL katika suala zima akaunti ya ESCROW na tuhuma za rushwa kwa wamiliki wake. 
3. EWURA kuomba radhi watanzania na wabunge kwa kujaribu kuirudisha IPTL kwa jamii huku ikitambua wazi miaka 3 iliyopita IPTL ilikuwa kwenye kashfa nzito iliyozua mtafaruku ndani na nje ya Tanzania.
4. LHRC, inaikumbusha jamii nzima ya watanzania, waheshimiwa wabunge, viongozi wa dini na vyama vya siasa kuungana pamoja kwa ajili ya maslahi ya umma katika kukata kusudio hili la kuongezewa leseni ya kuzalisha umeme nchini wakati kampuni tajwa imetiliwa shaka ya kuwa na dosari nyingi.
5. Serikali kutoa majibu na ufafanuzi wa utekelezwaji wa maazimio ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania juu ya kampuni ya IPTL. 
6. Serikali kupitia taasisi zake kuacha kufanya mazingaombwe kwa wananchi kwa kuwashirikisha katika shughuli ambazo hawajui misingi yake na badala yake wawe wazi katika hatua zote za makubaliano na wawekezaji.
Mwisho; Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinaamini vyombo vya habari vitakuwa mstari wa mbele kukumbusha namna Bunge na wadau wengine walivyosimama kidedea kuipinga kampuni ya IPTL baada ya kuibuka kwa sakata la ESCROW.

Imetolewa Alhamisi Juni 8, 2017

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji

No comments