Breaking News

TUGHE, OCEAN ROAD KUENDELEA KUSHIRIKIANA KUBORESHA MASLAHI YA WATUMISHI

Dar es salaam 
Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) kimesema kuwa kitaendelea kushirikiana kwa karibu na Uongozi wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road ili kuboresha maslahi ya Watumishi wake pamoja na kuchangia katika ustawi wa Taasisi hiyo. 

Ahadi hiyo imetolewa na Makamu Mwenyekiti wa TUGHE Taifa, Dkt. Jane Madete alipokuwa Mgeni Rasmi wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa TUGHE Tawi la Taasisi ya Saratani ya Ocean Road ( ORCI) uliofanyika leo Ijumaa tarehe 27 Septemba 2024 Jijini Dar es salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa TUGHE pamoja na wale wa kutoka katika Menejimenti ya Taasisi hiyo.

 Pia Dkt. Madete katika hotuba yake aliwasisitiza viongozi wa Tawi hilo kuendelea kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kujiunga na TUGHE ili kuongeza uelewa kwa watumishi wengi kujiunga na Chama. Aidha aliongeza kwa kusema kuwa Chama kimezipokea changamoto zote zilizowasilishwa na Viongozi na kuahidi zitashughulikiwa
Akitotoa salamu katika Mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa ORCI, Dkt. Julius Mwaiselage amekipongeza Chama kwa kazi nzuri wanazofanya na kuahidi kuendelea kudumisha ushirikiano uliopo kwani TUGHE imekuwa msaada mkubwa kwao katika maeneo mengi ikiwemo katika kuleta utulivu wa Taasisi na watumishi wote kuwa na ufanisi kazini.

Mkutano huo pamoja na mambo mengine ulikusudia kutoa mrejesho wa taarifa mbalimbali, Wanachama kufanya uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi mbalimbali, kukumbushana masuala muhimu ya ki utumishi pamoja na kuwaaga na kuwapongeza waliokuwa wanachama wenu wanaomaliza Utumishi wao



No comments