Breaking News

Dk. Shein Afunguwa Maonesho Siku Ya Chakula Duniani Zanzibar

Na waziri yakoub
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa katika kipindi cha hivi karibuni dhamira njema ya kuwapa eka tatu wananchi kwa ajili ya kilimo iliyooneshwa na uongozi wa Serikali tangu awamu ya Kwanza hadi hii ya Saba, imeanza kuharibiwa na baadhi ya wananchi kwa kuziuza eka hizo na wengine kuzikata viwanja vya kujenga nyumba na kuwauzia watu.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ufunguzi  wa maonesho ya Siku ya Chakula Duniani, yaliofanyika huko Kizimbani na kuhudhuriwa na wananchi pamoja na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, Mama Mwanamwema Shein na viongozi wengine wa vyama vya siasa na Serikali.

Katika hotuba yake, Rais Dk. Shein alisema kuwa kitendo hicho si kizuri kwani kinavunja mwelekeo wa azma ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 sambamba na kupelekea vizazi vijavyo kukosa sehemu za kilimo na hatimae kuagiza vyakula nje ya nchi.
Aliongeza kuwa ipo haja ya kuzingatia matumizi mazuri ya ardhi ndogo iliyopo kwa kutenga maeneo ya kilimo, maeneo ya makaazi na shughuli nyengine za kiuchumi sambamba na kuzingatia sheria za Mipango Miji na Vijiji.

Aliongeza kuwa hivi sasa Zanzibar ina watu milioni 1.4 hali hiyo inachangia kuwa na matrumizi makubwa ya ardhi hasa kwa ajili ya makazi na kupnguza ardhi ya kilimo, hivyo wananchi wanapotaka kujenga ni vyema wakapeka maombi yao katika Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira ili waelekezwe taratibu ziliopo.
Alisema kuwa hivi sasa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kufanya Mapinduzi ya Kilimo kwa kukifanya kilimo kuwa cha kisasa na cha kitaalamu hatua ambayo imeanza kuzaa matunda kwa kuongezeka kwa kiwango cha mavuno na mazao mbali mbali hasa mazao ya chakula yanayolimwa hapa nchini.

No comments