Breaking News

Sheikh Jalala Na Askofu Banza Wamuenzi Imam Hussein kwa kuzindua Mpango Wa Kugawa Maji Na Vipeperushi Bure.

Maulana Sheikh Hemed Jalala, Mchungaji kanisa la Tanzania Outreach Ministries Banza Suleiman na Mwenyekiti wa Kata ya Kigogo Mbuyuni Bw. Hassan Nguogani wakikata utepe kuzindua programu ya kugawa maji na vipeperushi burejijini Dar es salaam
Maulana Sheikh Hemed Jalala akiongea na waandishi wa habari ambao hawapo pichani mara baada ya kuzindua programu ya kugawa maji na vipeperushi bure mapema leo jijini Dar es salaam.
Mchungaji wa kanisa la Tanzania Outreach Ministries Banza Suleiman akitoa ufafanuzi wa jambo katika uzinduzi wa kugawa maji na vipeperushi bure zoezi lililofanyika mapema leo Masjid Al Ghadiir Kigogo Dar es salaam.
Mwenyekiti wa Kata ya Kigogo Mbuyuni Bw. Hassan Nguogani akiongea na waandishi wa habari ambao hawapo pichani mapema leo jijini Dar es salaam.
Maulana Sheikh Hemed Jalala akigawa maji kwa baadhi ya wakazi wa kata ya kigogo Mbuyuni mara baada ya kuzindua programu ya kugawa maji na vipeperushi bure jijini Dar es salaam.

Dar es salaam.
Waislam wa dhehebu la shia katika kuelekea siku ya Ashura Leo tarehe 10 ya muharram ambao ni sawa na mwezi wa kwanza katika kalenda kiislam wamezindua program ya ugawaji maji na vipeperushi bure iliyofanyika katika msikiti wa kigogo jijini Dar es salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo msikitini hapo Sheikh Jalala amesema kuwa zoezi hili la kugawa maji linaendana sambamba na kumuenzi Imam Hussein ambaye ni mjukuu wa pili wa Mtukufu Mtume Mohamad ambaye alifariki kwa kuwatetea wanadamu bila kuangalia itikadi zao za kidini, kikabila wala maumbile.

Sheikh Jalala alisema imam hussein amekuwa ni alama kwa dunia kwa kukubali yeye kufa ili watu wapate amani pamoja na kutendeana mema ikiwemo kupendana, kuhurumiana kuheshimiana na alithubutu kuyafanya hayo wakati huo ambao mema yalipungua katika dunia na hakukuwepo amani miongoni mwa wanadamu hao na matokeo yake yalikuwa ni ugomvi na chuki ndani ya kizani hicho.

Alisema Imam Hussein anatufundisha watanzania kuwa ni watu wenye huruma, upendo ushirikiano na amani tuliyopewa kama nuru yetu Watanzania, ndiyo maana msikiti huu umeamua kuanzisha program kama hizi ikiwemo kuwatembelea wagonjwa, kujitolea damu kwa hiari, kwenda kuwapa moyo wafungwa pamoja na kuwaona na kuwapa misaada watoto yatima ikiwa ni miongoni mwa njia za kumuenzi Imam huyo aliyejitoa kwa ajiri ya wanadamu.

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa kanisa la Tanzania Christian Outreach Ministries Mchungaji Banza Suleiman alisema kitendo kilichofanywa na msikiti huo ni chema na kinapaswa kuungwa mkono na kila Mtanzania anaependa maendeleo kwani maisha yetu wanadamu yanategemea maji kwa kiasi kikubwa, hivyo ili kumuunga mkono Rais Magufuli kufikia kuwa na uchumi mzuri wa viwanda ni lazima watu wawe na maji ya kutosha ili waweze kufanya kazi ipasavyo.

alisema mungu anambariki anaetoa hivyo kwa kujitolea huko mungu awabariki sana na hata serikali itafurahi kwa kuona taasisi za kidini zipo kwa dhumuni la kuwajari wananchi wake kama kitendo kilichofanywa na msikiti huo, pamoja na wananchi wa maeneo hayo wataona ni jambo jema kutokana na maisha ya mwanadamu yanategemea maji hivyo bila maji hakuna maisha.

Nae Mwenyekiti wa Mtaa Kigogo Mbuyuni Bw. Hassan Nguogani alisema wanaishukuru taasisi Shia kwa kuchangia maendeleo ya kata hiyo kwa kiasi kikubwa kwani imekuwa ikijitolea mambo mengi kama matibabu bure kwa wagonjwa, kusaidia watoto yatima katika kata hiyo kama madaftari na vifaa mbalimbali vya shule kwa wanafunzi na huduma nyingine nyingi.

Aidha Bw.Nguogani aliongeza kuwa taasisi hiyo imekuwa mstari wa mbele katika kusaidia juhudi za kimaendeleo kama kupanda miti, kufanya usafi maeneo ya kata hiyo, kuchangia ujenzi mbalimbali katika kata hiyo.

Alisema taasisi hiyo imekuwa itatoa misaada na kusaidia kufanya majukumu mengi ambayo kimsingi mengine utekelezwa na sreikali lakini taasisi hiyo wamekuwa wakijitolea hivyo kuwanufaisha wakazi wa kigogo na nifahari sana kwa uwepo wa msikiti huo mahali hapo.

No comments