Breaking News

SHEIKH JALALA ATUMA SALAM ZA KHERI NA FANAKA YA KUZALIWA YESU KWA WAKRISTO WOTE


TAARIFA KWA UMMA

Amani ya Mwenyezimungu iwe juu yenu nyote.Salam hizi za Mkono wa Krismas kwa ndugu zetu Wakristo wa Tanzania na Wakristo wote wanaosheherekea Mazazi (Kuzaliwa) kwa Nabii Issa (a.s) Mtume wa Mungu kwa ndugu zetu wakristo ni Yesu Kristo.

Mkono huu wa Kristmass, Mkono huu wa Eid ni Mkono uliobeba Umoja, ni mkono uliobeba Mshikamano ni Mkono wa Eidi, ni mkono wa Krismaa uliobeba amani na Maelewano. Lakini kubwa zaidi la kujiuliza na huenda wengi wakajiuliza swali hii kwamba kwanini Viongozi wa Dini wa Kiislam katika siku hii ya kuzaliwa Yesu Kristo au Nabii Issa (a.s) kwa Wiaslam, viongozi hawa wa Kiislam hususan Wafuasi wa Madhehebu ya Ahlulbayt (a.s) au Mashia watoe Mkono wa Krismas,mkono wa kheri,

mkono wa Baraka kwa ndugu zao wakristo Watanzania na wa Dunia kwa ujumla ni kwasababu chache za harakaharaka nitakazozieleza
Sababu ya kwanza tutambue sisi Waislam na ndugu zetu Wakristo sote tunakusanywa na neon moja kwamba sisi ni Waumini,

sote tunamuamini Mungu mmoja ambae ndie aliyeumba Mbingu na ardhi na akawaumba wanadam wote hilo la kwanza, Sote tunaamini kwamba kuna vitabu vya Mungu vilivyoshushwa hapa duniani, tunaamini uwepo utumwa mitume wa Mungu na vilevile tunaamini siku ya mwisho.

Kwahivyo kuyaamini haya yanatukusanya sisi watanzania Waislam na Wakristo chini ya mwamvuli mmoja wa imani, kwahivyo leo hii waislam tunapotoa mkono wa Krismas, mkono wa eid kwa ndugu zetu wakristo ni kwasababu ni waumini wenzetu katika kumuamini Mungu mmoja, katika kuamini siku ya mwisho na katika kuamini mitume waliotumwa na kutuletea ujumbe hili la kwanza.

La pili kwanini mkono wa Krimsaa kwa ndugu zetu Wakristo, ni kwasababu sisi wote tunakusanya na anuani ya Utanzania, Waislam tulioko hapa ni Watanzania, wakristo tulioko hapa ni Watanzania, kama sote ni watanzania ni wajibu wetu sote kuilinda Tanzania yetu. Kama sisi Wislam na Wakristo ni Watanzania ni wajibu wetu umoja na mshikamano wetu kama Watanzania, kama sisi sote ni watanzania ni makosa makubwa kufungua mwanya wowote wa mvutano kati ya Waislam na Wakristo hapa Tanzania, kwanini kwa sababu sote tunakusanywa ni Utanzania.

Kwasababu sisi sote ni watanzania ni lazima tuwe na sifa ya kuvumiliana, itikadi zetu, fikra zetu na mitazamo yetu isitugawanye kwa kuwa sisi tunakusanywa na neon Utanzania,Na Mtume Muhammad (s.a.w.w) kwa sisi waislam anasema “kupenda inchi yako ni katika imani” kwahivyo leo hii sisi kama Viongozi na kama Waislam na kama Waislam Shia Ithnasheriya tunapotoa Mkono wa Krisma, mkono wa Baraka na mkono wa Eid kwa ndugu zetu Wakristo moja ni kuenzi huu Utanzania tuliokuwanao ambao ni kitu muhimu na ni kitu kikubwa,Lingine ni kwanini tunatoa mkono wa Krismas,

ni kwasababu sisi Waislam, Dini ya Uislam ni dini ya Mapenzi, Dini ya Uislam ni dini ya kufahamiana, Dini ya Uislam ni dini ya amani, Dini ya Uislam ya kupendana, anaeueleza Dini ya Uislam sio dini ya kupendana huyo hajauelewa Uislam.

Kwahivyo Uislam ni dini ya Mapenzi, ni dini ya Maelewano ni dini ya Maelewano,Mtume Muhammad (s.a.w.w) anatufunza siku zote anasema “ penda watu wapate kile ambacho unachopenda ipate nafsi yako” kwahivyo Uislam ni dini ya upendo, uislam ni dini ya Maelewanoni dini ya masikilizano leo hii tunapotoa mkono wa Baraka na mkono wa kheri na fanaka katika Eid ya Krismass malengo makubwa ni kuwaonyesha ndugu zetu wakristo kwamba Uislam ni dini inayompenda kila mtu, Uislani dini iliyohimiza ujirani mwema na ujirani huu mwema hauwezi kudhibitika wala kufanyika pasi na watu kupendana.

Kwahivyo mkono huu wa Krismass ni mkono wa kuwaonyesha ndugu zetu Wakristo Wayanzania kwamba Uislam ni dini ya mapenzi, kwamba uislam ni dini ya kuelewana, Sayyidina Ali (a.s) kiongozi baada ya Mtume Muhammad (s.a.w.w) anawausia watoto wake anawambia “Hala hala nawahusieni majirani” Sayyidina Ali (a.s) alipokuwa anawahusia watoto wake swala la Majirani, hajawaambia Majirani Waislam, hajawaambia Majirani wachamungu la, kawaambia Majirani yaani majirani wote ima wachamungu, Wakristo, Waislam na hata wasiokuwa na Dini.

Kwahivyo kitendo cha leo cha sisi kutoa Mkono wa Krismass, mkono wa Kheri na Baraka kwa ajili ya ndugu zetu watanzania wasiokuwa Wiaslam ni kutaka kuwaonyesha kuwa Uislam ni dini ya mapenzi uislam ni dini ya maelewano.Nukta nyingine muhimu kwanini Mkono wa Krismass,mkono wa Kheri na Baraka kwa ndugu zetu Wakristo kwa sababu hakuna uadui kati ya Uislam na Ukristo, hakuna Uadui kati ya Waislam na Wakristo,

Ukimsoma Mtume Muhammad (s.a.w.w) na ukiisoma Qur’an yetu na ukisoma mwenendo wa watu waliokuja baada ya mtume Muhammad (s.a.w.w) utapata yakwamba wanavyoueleza Uislam, Uislam na Ukristo sio uadui kati yao bali ni Udugu na maelewano kati yao.

Iangalie Qur’an inavyowasemesha Wakristo inawaitaje, inawaita “Ahlul Kitabu” enyi watu waliopewa Injili, enyi watu mliopewa Taurat, enyi watu mliopewa Zaburi hivi ndivyo Qur’an inavyowasemesha Wakristo, kwahivyo Mkono huu wa Kheri na Baraka ni kuonyesha ya kwamba hakuna Uadui hata kidogo kati ya Uislam na Ukristo, kati ya Waislam na Wakristo.

Ukiisoma Qur’an, Qur’an ina sura nzima inayoitwa suratul Mariam yaani sura ya Mariam, mariam ambae kwa ndugu zetu Wakristo wanamwita “Bikira Maria” sisi kwetu Waislam tunamwita “Mariam Mtakatifu” ni sura nzima inayobeba jina la Mariam, kwahivyo lau Uislam ungelikuwa na Uadui na Ukristo kusinge kuwa na sura inayoitwa sura ya Maria.

Vilevile ndani ya Qur’an kuna sura ya Ruum yani sura ya Roma, Roma ni Wakristo ndani ya Qur’an, na Waislam wanaisoma sura hiyo kila siku ya asubuhi na mchana
Mwisho nimalizie kwa nukta yakwamba Kitendo cha sisi kutoa Mkono wa Kheri ya Krismass kwa ndugu zetu Wakristo watanzania ni kuonyesha yakwamba Uislam ni dini ya Amani, Uislam ni dini inayopenda watu wakae vizuri, Uislam ni dini inayopenda mahusiano mazuri kati yao na ndugu zao Wakristo,

na kwamba Uislam katika vitu inavyovipiga vita ni kitu kinachoitwa Ugaidi, Uislam na Ugaidi ni vitu viwili tofauti, ni kuontesha ya kwamba Uislam hauna kitu ukatili kwa wasiokuwa Waislam
Kitendo hiki cha kutoa mkono wa Krismas kwa ndugu zetu Wakristo ni kuonyesha kwamba Uislam hauna chinja chinja kwa Wakristo, Uislam hauna ukatili kwa Wakristo,

Uislam ni amani na maelewano kwa Waislam na wasiokuwa Waislam.mwisho niwatakie ndugu zetu wakristo Watanzania Eid njema, Krismass njema ya kusheherekea kuzaliwa Yesu Kristo au Nabii Issa (a.s).

Na vilevile ni itakie amani serikali yetu ya awamu ya tano ambayo imeweza kutufikisha hapa kwa utulivu na kwa maelewano sisi Waislam Watanzania na Wakristo wa Tanzania, na ninamuomba Mwenyezimungu Serikali hii awape hekima, awape busara ili waendelee kutuongoza kwa salama na kwa amani na

vilevile mwenyezimungu nchi hii azidi kuboresha maelewano kati yetu sisi Waislam na kati ya ndugu zetu Wakristo, na yeyote ambae anania ya kuleta chokochoko ya kuvunja amani hii, basi chokochoko yake isiweze kuingia katika nchi yetu ya Tanzania na katika taifa hili, Mungu azidishe kulibakiza Taifa hili la Tanzania katika Amani na kisiwa cha amani na mahala pa maelewano.Asanteni sana na Mungu awabariki.

Imetolewa Na:

Kiongozi Mkuu wa Waislam Dhehebu la Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala

No comments