Breaking News

MGANGA WA KIENYEJI AUAWA AKIMBAKA MGONJWA WAKE SHINYANGA

Kamanda wa jeshi jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga ACP Muliro Jumanne akionesha vifaa vya uganga vya waganga wa kienyeji 22 waliokamatwa wakidaiwa kujihusisha na upigaji ramli chonganishi hivi karibuni-Picha kutoka maktaba.
 
Wananchi wenye hasira kali wamemuua mganga wa kienyeji aliyejulikana kwa jina la Kashinje Kashinje(55), mkazi wa kijiji cha Singita kata ya Usanda wilayani Shinyanga kwa kumshambulia kwa silaha za jadi wakati akijaribu kumbaka mwanamke mwenye umri wa miaka 20 (jina linahifadhiwa) aliyefika nyumbani kwa mganga huyo kupata tiba ili apate mtoto.

Mganga huyo alitaka kumbaka mgonjwa wake  mkazi wa kijiji cha Ishinabulandi baada ya kumlewesha na dawa za kienyeji.

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga Muliro Jumanne amesema tukio hilo limetokea Novemba 29,2016 saa tano asubuhi nyumbani kwa mganga huyo..

Amesema mganga huyo alifariki dunia baada ya kushambuliwa na wananchi waliojichukulia sheria mkononi baada mganga huyo kujaribu kumbaka mwanamke huyo.


Kamanda Muliro amesema chanzo cha tukio hilo ni tamaa za kimwili na uongo wa kimatibabu wa kutaka kumuingilia kimwili mgonjwa wake baada ya kumlewesha kwa dawa za kienyeji lakini mgonjwa alipiga kelele akiomba msaada ndipo wananchi wakafika eneo la tukio.