Breaking News

TAMKO LA WIZARA KUHUSU MATUMIZI NA USAMBAZAJI WA VILAINISHI KWA AJILI YA UDHIBITI WA MAAMBUKIZI YA UKIMWI

logo 
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imekuwa ikitekeleza afua mbalimbali za mapambano dhidi ya maambukizi ya VVU nchini ambazo zimepelekea kupungua kwa viwango vya maambukizi ya VVU kitaifa kutoka wastani wa asilimia 7 mwaka 2007-2008 hadi kufikia asilimia 5.1 mwaka 2011-2012. Mafanikio haya yamefikiwa kutokana na ushirikiano wa karibu kati ya Wizara na wadau mbalimbali wa maendeleo pamoja na wale wa utekelezaji wa moja kwa moja wanaofanya kazi na mikoa yote Tanzania bara. Aidha kumekuwa na uitikiaji mzuri kutoka kwa wananchi katika utekelezaji wa afua hizo.

Sambamba na mafanikio haya, tafiti mbalimbali hapa nchini zimethibitisha kuwepo kwa kiwango cha juu cha maambukizi ya VVU miongoni mwa makundi maalum yaliyo katika hatari zaidi ya maambukizi kuliko kiwango kilichopo miongoni mwa jamii ya kawaida. Makundi haya ni pamoja na Wanawake wanaofanya biashara ya ngono ambayo maambukizi ya VVU ni asilimia 26, Watu wanaojidunga sindano za madawa ya kulevya (asilimia 36) na Wanaume wanaoshiriki ngono baina yao (asilimia 25). 
Aidha, makundi haya yamekuwa na muingiliano wa karibu sana na wana jamii ya kawaida, na hivyo kupelekea hatari ya kutofanya vizuri katika udhibiti wa maambukizi ya VVU nchini.

Hali hii ilisababisha kuwepo na umuhimu wa kuongeza nguvu katika afua mbalimbali za kukabiliana na ongezeko la maambukizi ya VVU miongoni mwa makundi haya, pamoja na jamii ya kawaida ili kudhibiti VVU. Kwa mantiki hiyo, Wizara kwa kushirikiana na wadau mbali mbali walikubaliana mikakati mahsusi ya kutoa huduma bora na rafiki kwa watu wa makundi maalum kwa kuzingatia sheria, taratibu, mila na desturi za taifa letu.

Pamoja na nia njema na jitihada za pamoja baina ya Wizara na wadau katika mapambano dhidi ya UKIMWI, imebainika kwamba baadhi ya wadau wanaotekeleza shughuli za makundi maalum wamekuwa wakikiuka taratibu za kiutendaji hasa suala la kuihusisha Wizara na Mikoa husika wanakofanyia kazi kuhusu uanzishwaji na/au utekelezaji wa baadhi ya shughuli wanazozifanya. Aidha pia katika baadhi ya maeneo, wadau hao wamekuwa wakitekeleza shughuli ambazo ziko kinyume na makubaliano waliyoingia na Wizara ya Afya.

Miongoni mwa shughuli zinazokinzana na mila na desturi zetu ni pamoja na usambazaji wa vilainishi. Ni kweli kuwa Wizara imezuia usambazaji wa vilainishi na tayari tumewasiliana na wadau hao ambao wameahidi yafuatayo:
  • Kukusanya vilainishi vilivyokuwa vimesambazwa na kuhakikisha kuwa vinateketezwa
  • Imekubalika pia kuwa wadau kwa kushirikiana na Wizara watakaa pamoja na kuangalia endapo pana fedha ambazo zingetumika kununua vilainishi, basi fedha hizo ziweze kupangiwa matumizi stahiki kulingana na vipaumbele vya Wizara na taifa kwa ujumla.
Wizara inawapongeza na kuwashukuru wadau wote kwa jitihada za dhati zinazoendelea kutekelezwa na katika kusimamia kikamilifu miongozo inayotolewa na Wizara yenye lengo la udhibiti wa ugonjwa wa UKIMWI.
Imetolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
19 Julai 2016